JE, WAJUA KUWA MUDA UNAYOYOMA?

Mwanadamu anayo maswali mengi ya kujiuliza kuhusu wakati anaoishi hapa duniani tangu kuzaliwa hadi umri alionao. Mtu mwenye akili na ufahamu lazima atajiuliza na kujitathimini kuwa amefanya nini katika umri alionao akiwa ni kijana au mzee.
Kama tunavyojua ya kuwa muda unakwenda kasi sana na kadiri siku zinavyosogea ndivyo maisha ya mwanadamu yanavyoelekea ukingoni.
 Kuna wakati natafakari juu ya maisha yangu na muda nilionao hapa duniani  na kujiuliza maswali mengi kila iitwapo leo. Siku zinaenda, miaka inasogea na majira hayasimami, ni kama ilivyo dunia inavyojizungusha katika mhimili wake bila kupumzika tukapata kuuona usiku na mchana ndivyo muda unavyosogea au unavyoyoyoma. Lazima nijiulize nimefanya nini katika umri nilio nao tangu nimeanza kupata ufahamu aidha nimeutumia muda wangu kwa faida au hasara. Ni vyema kutambua kuwa kila siku ni siku mpya na siku hazifanani katika muda wa mwanadamu kuishi hapa duniani unapoamka asubuhi sio kama jana bali umekuwa na umri mwingine na muda wako wa kuishi unaendelea kupungua huenda na nguvu zako zinaendelea kupungua kulingana na umri unavyosogea.  Ni vyema ndugu yangu ukagundua kuwa tuna muda mchache sana wa kuishi hapa duniani  wakati jambo ambalo wengi wetu tumelisahau na wakati mwingi tunahangaika tukisema tunatafuta maisha tungali tunapoteza nguvu nyingi na muda bila kujua. 

Basi angalieni sana jinsi mnavyoenenda; si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima; mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu. Kwa sababu hiyo msiwe wajinga, bali mfahamu ni nini yaliyo mapenzi ya Bwana. Waefeso 5:15-17

Ni vigumu mtu kugundua mapema kuwa anapoteza muda ila hilo linaonekana mara tu anapoona umri umesogea na hakuna alichokifanya katika maisha kinachoweza kumsaidia katika wakati nguvu zake zimeanza kupungua.
"Pale unapopata akili ndipo unagundua kuwa ulikuwa umepotea."
Mara nyingi tunapoteza muda katika mambo yasiyo ya msingi au kuleta faida kwenye maisha tunaacha kufanya mambo muhimu ya uzalishaji ambayo yanaweza kutunufaisha katika maisha tunayoishi na kwa vizazi vyetu vijavyo.
Kwa sababu ya ujinga na kukosa maarifa tunaangamizwa kwa kutoielewa teknolojia inayokuwa kwa kasi katika dunia ya sasa kwa sababu tunapumbazwa na mambo ambayo wengine wameyatengeneza na kila siku yanawapa faida wakati sisi tunaangamia. "Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa; Hosea 4:6" 
Kukosa maarifa siyo kukosa mtaji wala siyo kukosa ajira au kazi fulani bali ni kutokujua ufanye nini kulingana na majira na nyakati unazoishi. Ni kutokuwa na hekima na ufahamu ni pamoja na kuchukulia mambo kikawaida kawaida tu.
Kuna umuhimu wa kujitambua katika nyakati tunazoishi kujua kuwa kuna mambo muhimu ya kufanya na kuachana na mambo ya kipuuzi yasiyo na faida katika maisha yetu.
Mtu anayejitambua atapangilia maisha yake kulingana na muda alionao akiukomboa wakati kwa kufanya mambo yenye tija na kuachana na yale yasiyo na maana au yenye kumpotezea muda kama kukaa vijiweni, kumbi za starehe, kupoteza muda kwenye mitandao ya kijamii, kutumia muda mwingi kwenye Tv na mambo yanayofanana na hayo. 
Ndugu yangu na rafiki, ni vyema kuukomboa wakati katika zama hizi tulizonazo na kuweka bidii kwenye mambo muhimu katika maisha na kuepukana na umaskini ambao ni janga kubwa sana linalotesa watu wengi sana duniani hivi leo.
Jitambue wewe ni nani, komboa wakati na utimize malengo yako ungali na nguvu, epuka kupoteza muda bali uutumie vizuri kwa faida.
Ni mimi rafiki yako
Innocent Moshi
0658 185 444/ 0625695550
E-mail: innommoja2@gmail.com

Comments

Popular posts from this blog

NI KWA NINI MAONO YAKO HAYAFANIKIWI?

UKIACHA TABIA HII UTAWEZA KUTIMIZA MALENGO YAKO.

JE UNATAFUTA MTAJI?